Recent Posts

Tegete mechi 3 goli 3 VPL

Straika wa zamani wa Yanga SC, Jeryson Tegete ‘Jerry’ ameanza vizuri msimu huu akiwa na klabu ya Mwadui FC ya Shinyanga. Tegete ambaye alianza kuichezea Mwadui katika mchezo wa suluhu-tasa dhidi ya Coastal Union katika uwanja wa Mkwakwani, Tanga akitokea Falme za Kiarabu ambako alichelewa usajili wa huko na kurejea nchini.

Alifunga goli lake la kwanza msimu huu katika ushindi wa Mwadui FC dhidi ya JKT Ruvu katika dimba la Mwadui Complex wiki iliyopita. Mshambuliaji huyo wa zamani wa timu ya Taifa Stars alifunga magoli mengine mawili katika ushindi wa 3-1 ambao Mwadui FC iliupata Alhamis hii dhidi ya JKT Mgambo. Tegete amefunga magoli yote matatu katika uwanja wa Mwadui Complex.

Mchezo wake wa nne msimu huu utakuwa dhidi ya vinara na mabingwa watetezi Yanga SC ambayo ni timu ya zamani ya Jerry. Tegete aliichezea Yanga kuanzia msimu wa 2008/09 hadi msimu uliopita. Aliachana na Yanga baada ya mkataba wake kumalizika na hakika sasa Jerry ana furahia maisha ya mpira nje ya klabu iliyompatia mataji manne ya ligi kuu.

“Tunamshukuru mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kupata ushindi huu, Mechi ilikuwa ngumu sana lakini vijana wangu walikuwa watulivu, wamefuata maelekezo na hatimaya tumeweza kupata ushindi huu mzuri. Jerson Tegete amefunga magoli mawili (Dakika ya 8’ na 25’ kwa njia ya penati) na linguine limefungwa na mlinzi wa kulia Malika Ndeule kwa shuti la zaidi ya mita 35” anasema Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ kocha mkuu wa Mwadui FC.

No comments