Recent Posts

HUU NI WAKATI SAHIHI WA POPPE KUJIVUA MAJUKUMU YAKE SIMBA SC, AMESHINDWA VIBAYA



Zacharia Hans Poppe, mwenyekiti wa kamati ya usajili Simba SC
Zacharia Hans Poppe, mwenyekiti wa kamati ya usajili Simba SC
Na Baraka Mbolembole, Dar es Salaam
Wakati pambano la Yanga SC na Toto Africans likiendelea katika uwanja wa Taifa, Dar es Salaam baadhi ya mashabiki wa klabu ya Simba SC walikuwa ‘wakisonokea’ utawala wa klabu yao kwa kitendo cha kuwaacha wachezaji vijana ‘mazao ya klabu’ na kuwasaini wachezaji wapya ambao si wa kiwango cha juu. Mfungaji namba moja wa Toto ni  kijana Miraj Athumani ambaye alitimiza goli lake la tatu msimu huu katika kichapo cha 4-1 kutoka kwa Yanga siku ya jana Jumatano.
Edward Christopher tayari amefunga mago mawili msimu huu, wakati Abdallah Seseme, Hassan Khatib wameendelea kucheza vizuri katika kiungo ( Seseme) na safu ya ulinzi ( Khatib). Vijana hao wanne walikuwa sehemu ya timu B ya Simba SC ambayo ‘ ilitingisha’ Tanzania Bara mwaka 2012.
Simba awali ilikuwa na mtazamo wa kutumia wachezaji inaowazalisha yenyewe. Kwa maana ya kiushindani na kibiashara lakini mtazamo huo umeshindikana kutokana na ‘propaganda’ za viongozi wa juu wa klabu hiyo.
Leo hii Simba haipati huduma ya Shomari Kapombe, Ramadhani Singano na badala yake vijana hao U23 wanaichezea Azam FC . Ni sababu za kimaslahi zilizowaondoa ndani ya klabu hiyo. Nimewahi kuandika mara nyingi kuhusu mapungufu ya kiutendaji ya mwenyekiti wa kamati ya usajili wa klabu hiyo, Zacharia Hans Poppe. Simba imekuwa ikitumia kiasi kikubwa cha pesa kuwasaini wachezaji wa ndani na nje ya nchi bila kuzingatia aina ya wachezaji husika na mahitaji ya timu kiujumla.
Sijawahi kuwa upande wa Poppe kwa kuwa naamini kufanya hivyo ni sawa na kuendelea kushabikia hatua za klabu kurudi nyuma badala ya kusonga mbele. Niseme wazi kuwa Singano hakupaswa kuondoka Simba kwa sababu tu klabu ilishindwa kumpatia kiasi cha pesa alichohitaji ili kusaini mkataba mpya.
 Inasemekana kuwa mchezaji huyo alihitaji kiasi cha milioni 50 lakini klabu iling’ang’ania kumsaini kwa milioni 30 na baada ya mchezaji kukataa dau hilo yakatengenezwa mazingira ya kumfunga kwa kigezo cha kuwa na mkataba nae, jambo ambalo halikuwa na ukweli.
Mchezaji ambaye klabu imemlea kwa miaka minne tena akiwa katika kiwango cha juu kama Singano hakupaswa kuachana na Simba. Yeye pia hakupenda lakini aliamua kuchagua maisha mengine Azam FC baada ya timu hiyo kumuheshimu. Kamati ya usajili ya Simba imeshindwa kuwaheshimu wachezaji vijana ambao kwa hakika hivi sasa ndiyo walistahili kulipa fadhila kwa kuwapa taji au nafasi ya pili katika ligi kuu.
Klabu inakataa kumpatia Singano milioni 50 lakini ina uwezo wa kusajili ‘wachezaji magarasa’ kutoka nje ya nchi zaidi ya wawili. Hii yote ni kazi ya ‘Mr.Kazinyingi’ ambaye siku zote anaamini katika matumizi ya hela ili kujenga timu.
Bahati mbaya kwa Poppe kila wachezaji ambao wanaosajiliwa kwa gharama wanashindwa kuleta mabadiliko katika timu. Na wale ambao wamekuwa wakiachwa na kujiunga na klabu nyingine wamekuwa na mafanikio. Hii ni dalili ya kwamba Kamati hiyo ya usajili ya klabu ya Simba haiwezi kuitengeneza timu mpya ya ushindi kwa kuwa hawajui namna ya kutengeneza timu.
Jiulize tu, kwanini Kapombe, Singano, Christopher, Miraj, Seseme, Khatib, Wiliam Lucian leo hii wapo nje ya timu. Hawa ni vijana sita ambao walikuwa sehemu ya kikosi B kilichoshinda mataji matatu mwaka 2012/13 katika michuano ya Super8, Ujirani Mwema na Mapinduzi Cup baada ya utawala uliopita kuwapa nafasi vijana hao huku timu A ikipambana kushinda ubingwa wa ligi kuu.
Sijawahi kuona ‘taswira’ ya Simba kunyanyuka na kuleta ushindani katika ligi ikiwa chini ya Kamati ambayo mara zote inawaza muda wa usajili ufike ili ipate nafasi ya kuwatema wachezaji fulani na kuwasaini wachezaji wengine wapya hata kama hakuna ulazima wa kufanya hivyo.
Ibrahim Twaha ni kijana ambaye Simba ilimsaini kutoka Coastal Union akiwa na kiwango cha juu lakini baada ya kuumia Kamati ya usajili ya klabu ilimtazama kama ‘mzigo’ hivyo kama ilivyotoa kwa kundi la kina Miraji, Christopher, Singano, Khatib, Lucian na Seseme hakupewa mkataba mpya lakini sasa anaendelea kuonesha kiwango kizuri katika timu ‘dhaifu’ ya Coastal.
Vipi kuhusu kuachwa kwa Mrundi, Amis Tambwe, kijana mwingine Haroun Chanongo msimu uliopita. Poppe inawezekana hana ufahamu mkubwa kuhusu wachezaji anaokuwa akiwaacha ama kuwasaini. Pia anajitambulisha kama kiongozi asiye na uwezo wa kuwasaini wachezaji bora. Kwa hakika Kamati yake inaongoza kwa usajili wa wachezaji wa hovyo zaidi klabuni hapo, pia ni Kamati ya usajili iliyochemka zaidi kimaamuzi kwa kuwaacha wachezaji makini.
Simba itaendelea ‘kusafa’. Itahangaika sana na kamwe nadiriki kusema utawala wa sasa unaweza kumaliza miaka yao minne pasipo kushinda ubingwa wa ligi kuu kama tu watashindwa kufikia maamuzi magumu ya kumuondoa Poppe katika nafasi yake. Mara zote naamini kuwa ‘Mafanikio ndiyo kipimo sahihi cha ubora’ lakini bado sijayaona Simba tangu ikiwa chini ya Hans Poppe.
Tambwe, Elius Maguli, Christopher, Chanongo, Singano, Seseme, Miaraj, Khatib, Lucian, Kapombe, Twaha ni wachezaji 10 ambao hawakustahili kuachwa Simba SC. Pape Nd’aw, Danny Sserunkuma, Paul Kiongera, Donald Musoti, Emily Namubona, Simon Sserunkuma, Vicent Aghban, ni baadhi tu ya usajili usio na tija uliofanywa na kamati ya usajili ya Simba SC.
Huu ni wakati sahihi wa Poppe kujivua majukumu yake Simba na ajitolee kama mwanachama wa kawaida tu. Nasikia sasa ‘Jicho kama ngumi kuelekea dirisha dogo la usajili’. Timu gani kila baada ya kucheza gemu 5 inaomba muda wa usajili ufike….

No comments